Wizara
ya Mawasiliano Sayansi na Teknolojia inajiandaa kupeleka bungeni
muswada wa sheria ya makosa ya mtandao 2015 ambayo unaweza kuisoma kwa
kubofya hapa. Kama zilivyo sheria nyingi kabla ya kupitishwa wabunge
hupewa nafasi ya kuijadili na kufanya marekebisho pale penye mapungufu.
Baada ya kuipitia haraka haraka nimegundua baadhi ya vitu ambavyo
naamini havijakaa sawa na nimejaribu kuelezea kwa chini yake. Ni
matumaini yangu wabunge wetu wataipitia vizuri zaidi na kugundua mengi
ambayo sijayaona.
Endelea kusoma:
Kutoa
taarifa za uongo. 16. Mtu yeyote anayetoa taarifa, data au maelezo kwa
njia ya picha, uongo maandishi, alama au aina nyingine yoyote kwenye
mfumo wa kompyuta, endapo taarifa, data, au maelezo hayo ni ya uongo,
yanapotosha au yasiyo sahihi, atakuwa ametenda kosa, na akipatikana na
hatia atalipa faini isiyopungua shilingi milioni tatu au kutumikia
adhabu ya kifungo kisichopungua miezi sita au vyote.
Sheria
hii ina mapungufu, kumbuka kazi mojawapo ya mtandao ni kuelimishana na
katika kufanya hivyo takwimu nyingine zinazopatikana zinaweza zisiwe
kweli lakini kwa kutofahamu mhusika akazitumia. Lazima kiwepo kipengele
kinachomlinda mtu wa aina hii.
Unyanyasaji
kwa kupitia mtandao 23.-(1) Mtu hataanzisha au kukadimisha mawasiliano
yoyote ya kielektroniki kwenda kwa mtu yoyote kwa kutumia mfumo wa
kompyuta, kwa lengo la kurubuni, kulazimisha, kutisha au kunyanyasa au
kusababisha maudhi ya hisia. (2) Mtu akataye kiuka kifungu kidogo cha
(1) atakuwa ametenda kosa na atawajibika, iwapo atatiwa hatiani, kulipa
faini isiyopungua shilingi milioni tatu au kutumikia kifungo kwa kipindi
cha kisichopungua mwaka mmoja au vyote.
Haiingii
akilini mtu ambaye anatenda kosa kama hili kupewa kifungo cha mwaka
mmoja tu au faini ya milioni . Kuna watu wanajidhuru miili yao kwa ajili
ya manyanyaso ya mitandaoni kutoka kwa watu waliowaamini ambao baadae
wanasaliti uaminifu wao. Kuna haja ya kuongeza muda wa kifungo na kiasi
cha faini ikibidi iwepo na kipengele cha fidia kwa mhanga wa kosa hili.
Ukiukaji
wa haki bunifu 24.-(1) Mtu hatatumia mfumo wa kompyuta kwa lengo la
kukiuka haki bunifu zinazolindwa na Sheria nyingine yoyote. (2) Mtu
akatayekiuka kifungu kidogo cha (1) atakuwa ametenda kosa na akitiwa
hatiani, atawajibika iwapo ukiukaji – (a) hauhusiani na masuala ya
kibiashara, kulipa faini isiyo pungua shilingi milioni tano au kutumikia
kifungo kwa kipindi kisichopungua miaka mitatu au vyote; (b) unagusa
masuala ya kibiashara, kulipa faini isiyo pungua shilingi milioni
ishirini au kutumikia kifungo kwa kipindi kisichopungua miaka mitano au
vyote.
Sielewi
COSOTA, BASATA au Bodi ya Filamu wameshirikishwa kiasi gani katika
utungaji wa hiki kipengele. Kumbuka kutumia kazi ya mtu mwingine
kujiingizia kipato unamtia hasara, adhabu haijahusisha kufidia hasara
iliyosababishwa na ukikukwaji wa sheria hii badala yake imewekwa faini
ambayo ni rahisi sana kuilipa hasa kama umejineemesha vya kutosha
kupitia kazi yenyewe. Mfano: Wanaotoa nakala feki za bongomuvi
wanaingiza mamilioni kila siku kwa kuzisambaza ndani nan je ya nchi na
hata kuzikodisha hawawezi kushindwa kulipa faini rahisi hivyo.
Jaribio
la kufanya uhalifu 26.-(1) Pale ambapo mtu anayekusudia kutenda kosa
anaanza kutekeleza kusudio lake na anadhihirisha kusudio lake kwa
kitendo kinachoashiria kosa, isipokuwa hatekelezi kusudio lake kwa kiasi
cha kutenda kosa hilo, atachukuliwa kuwa ametenda kosa hilo. (2) Kwa
madhumuni ya kifungu hiki- (a) isipokuwa kwa kiasi cha adhabu
haitajalisha iwapo- (i) mkosaji anatenda yote ambayo ni muhimu kwa
utendaji wa kosa; au (ii) utekelezaji wa kusudio lake kwa ukamilifu
unazuiliwa na mazingira ambayo hayaingiliani na kusudio lake; au (iii)
anaacha kutekeleza kusudio lake kwa hiari yake mwenyewe; (b) kutokana na
sababu za mazingira yasiyojulikana kwa mhalifu haiwezekani kutenda
kosa. (3) Mtu yeyote anayejaribu kutenda kosa chini ya sheria hii atakua
ametenda kosa na akitiwa hatiani atawajibika kulipa faini isiyopungua
shilingi milioni moja au kifungo kwa kipindi kisichopungua miezi sita au
vyote.
Kula
njama ya kutenda kosa 27. Mtu anayekula njama na mtu mwingine kutenda
kosa chini ya Sheria hii, anatenda kosa na iwapo atatiwa hatiani,
atawajibika kulipa faini isiyopungua shilingi milioni moja au kutumikia
kifungo kwa kipindi kisichopungua mwaka mmoja au vyote.
Haieleweki
itajulikana vipi mtu ALIKUSUDIA kula hivyo kutoa mwanya kwa watu
kubambikiwa kesi pale wanapoenda kinyume na matakwa ya watu fulani. Hii
inatokea mara nyingi sana na tumeshuhudia ikithibitishwa watu wameuziwa
kesi huku wale wasio na wanasheria wazuri wa kuwatetea wakiishia
kuingizwa hatiani.
Ulinzi
wa miundo mbinu muhimu ya TEHAMA 28.-(1) Waziri anaweza, kwa amri
itakayochapishwa kwenye Gazeti la Serikali kuainisha mifumo ya kompyuta
kama miundombinu muhimu
(2)
Amri iliyorejewa chini ya kifungu kidogo cha (1) inaweza kuainisha
vigezo, miongozo na taratibu kuhusiana na- (a) usajili, ulinzi au
utunzaji; (b) usimamizi wa jumla; (c) kuingia, kuhamisha na kudhibiti
data; (d) kuhakikisha uwepo wa audilifu au uhalali wa data au taarifa;
(e) njia zitakazotumika kuhifadhi au kutunza data; (f) mipango ya
kudhibiti majanga iwapo kutatokea uharibifu; (g) namna na utaratibu wa
kuendesha ukaguzi; (h) jambo jingine lolote ambalo ni muhimu kwa ulinzi,
usimamizi na udhibiti wa data na rasimali nyingine. (3) Kwa madhumuni
ya kifungu
–
Waziri amepewa madaraka makubwa sana katika hili ikimpa nafasi ya
kuingia katika mifumo ya kompyuta na kufanya yaliyotajwa hapo juu.
Katika wakati tulionao kisiasa ambapo kuna wimbi kubwa la
wafanyabiashara katika siasa sitoshangaa mmoja ya mawaziri ambaye ana
maslahi kibiashara katika mawasiliano au biashara nyingine inayohusiana
na tasnia hii kutumia madaraka haya kujinufaisha au kuwanufaisha
washirika wake kupitia sheria hii. Ninadhani madaraka haya angepewa mkuu
wa kitengo cha Cyber Crime na sio MWANASIASA.
Kufifilisha
kosa 50.-(1) Bila kuathiri sheria nyingine inayotumika Tanzania Bara,
Mkurugenzi wa Mashtaka, muda wowote kabla ya mwenendo wa mahakama kuanza
na kwa kuzingatia tamko la kukiri kosa kwa hiari la mshitakiwa anaweza
kufifilisha kosa na kuamuru mtu huyo alipe kiasi cha pesa atakachokitaja
ambacho hakitazidi kiasi cha faini kwa kosa hilo.
(2) Amri ya kufifilisha kosa chini ya kifungu kidogo cha (1) itakuwa –
(a)
ya maandishi, ikiainisha kosa lililotendeka, kiasi cha fedha
zitakazolipwa na tarehe ya kufanya malipo ikiambatanisha tamko la
kukubali kosa lililorejewa chini ya kifungu kidogo cha (1);
(b) ni uamuzi wa mwisho na hautakatiwa rufaa; na
(c) na uwezo wa kutekelezwa katika namna sawa na amri ya Mahakama Kuu.
Naamini
rufaa ni haki ya kila mtuhumiwa anaeamini hakutendewa haki. Kusema
hukumu itokanayo na makosa ni ya mwisho bila haki ya rufaa ni kukiuka
haki ya msingi. Kuna haja ya kurekebisha hili.
NYONGEZA
Muswada
haujabainisha wafichuaji maovu “whistle blowers” wanalindwa vipi katika
sheria hii kutoka vipengele vinavyoonekana kuwalenga watu ambao ni
chanzo cha habari kwa kigezo cha “kutishia usalama wa nchi”. Nchi za
wenzetu wanaamini demokrasia ni pamoja na uhuru wa kufichua habari
ambazo zina manufaa kwa umma na wanatunga sheria za kuwalinda.
Hayo
ndio mapungufu niliyoyaona. Kama kuna una kingine ambacho unaamini
kinafaa kurekebishwa tafadhali weka katika comment..
Post a Comment